Thursday, November 8, 2012

CAF: orodha fupi ya wachezaji bora soka


 5 Novemba, 2012 - Saa 13:30 GMT
CAF
Wachezaji bora zaidi wa soka barani Afrika watatangazwa na CAF tarehe 20 Desemba
CAF imetangaza orodha fupi ya majina ya wachezaji ambao wamo katika nafasi nzuri zaidi ya kutwaa tuzo ya mchezaji bora zaidi barani Afrika.
Mshindi wa mwaka jana, Yaya Toure, anaongoza katika orodha hiyo yenye majina ya wachezaji 10, waliochaguliwa kutoka orodha ndefu ya wachezaji 34.

Mchezaji huyo kutoka Ivory Coast, ambaye ni kiungo cha kati wa timu ya Manchester City, ni kati ya wachezaji wanne wanaozichezea timu za Uingereza ambao huenda wakapata tuzo hiyo ya mwaka 2012.

Kiungo cha kati wa Chelsea, John Obi Mikel, mshambulizi wa Arsenal, Gervinho, Demba Ba wa timu ya Newcastle, ni kati ya wachezaji wengine wa ligi kuu ya Premier ambao wanawania tuzo hiyo.

Katika orodha hiyo, kuna wachezaji wengine ambao waliwahi kucheza Uingereza mwaka 2012.

Wachezaji hao ni aliyekuwa kiungo cha kati wa Arsenal, Alexandre Song, na ambaye sasa huichezea Barcelona ya Uhispania, na mshambulizi wa zamani wa Chelsea, Didier Drogba, ambaye anaichezea klabu ya China, Shanghai Shenhua.

Chris Katongo ni mchezaji wa pekee kutoka timu ya Zambia iliyoibuka mshindi katika mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika.

Mchezaji wa Morocco, Younes Belhanda, yumo katika orodha hiyo, kwa juhudi zake mapema mwaka huu, katika timu ya Ufaransa ya daraja ya kwanza, Montpellier.

Wanaowania tuzo hiyo, watapunguzwa hadi kufikia watatu, katika wiki ya mwisho ya mwezi Novemba.

CAF vilevile ilitangaza orodha fupi ya wachezaji watano, ambao wana nafasi ya kupata tuzo la mchezaji bora barani Afrika, kwa wachezaji ambao hucheza kandanda yao barani Afrika.

Katika ordha hiyo ni pamoja na Mohamed Aboutrika, kiungo cha kati kutoka Misri, na aliyecheza katika mechi ya Al Ahly ya klabu bingwa dhidi ya Esperance ya Tunisia, mchezo uliokwishwa kwa sare ya 1-1 siku ya Jumapili.

Tuzo hizo, ambazo zitakuwa pia ni kumpa zawadi kocha bora zaidi wa mwaka, na klabu bora zaidi mwaka 2012, zitatolewa kwa washindi tarehe 20 mwezi Desemba, katika ukumbi wa Banquet, katika ikulu ya rais, katika mji mkuu wa Ghana, Accra.

No comments:

Post a Comment